Baadhi ya vipodozi vilivyopigwa marufuku na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) TAKWIMU zilizotolewa na Taasisi ya Saratani Oc...
Baadhi ya vipodozi vilivyopigwa marufuku na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) |
TAKWIMU
zilizotolewa na Taasisi ya Saratani
Ocean Road (ORCI) tatizo la ugonjwa wa Saratani inayotokana na vipodozi
imeongezeka kutoka wagonjwa zaidi ya 2000 katika kipindi cha mwaka 2000 na kufikia 5,400 kwa sasa.
Pia
utafiti uliofanywa hapa nchini na Profesa Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Georgia,
Atlanta, Marekani, Kelly Lewis wa kitengo cha Sosholojia, kuhusu matumizi ya ‘mkorogo’
kwa wanawake nchini Tanzania, umebaini kwamba zaidi ya wanawake milioni sita wapo
kwenye hatari ya kuugua saratani kutokana na matumizi ya vipodozi.
Kadhalika
taarifa za utafiti huo zinaonyesha kwamba idadi ya wanawake wote Tanzania ni milioni
23 na kati yao asilimia 30 sawa na
milioni 6 wanatumia vipodozi vyenye kemikali hatari na madini ya Zebaki,
Hydroquinone pamoja na maji ya betri.
Kutokana
na matumizi hayo, Lewis anasema Tanzania ipo kwenye hatari ya ongezeko la
walemavu wa mtindio wa ubongo kwa wanawake wengi kuzaa watoto wakiwa kwenye
ulemavu huo huku wengi wao wakipoteza maisha kutokana na kukithiri kwa matumizi
ya vipodozi hivyo vilivyotengenezwa kwa kutumia kemikali zenye viambata sumu.
Zaidi
Prof. Lewis anasema asilimia 70 ya vipodozi hivyo huingizwa kutoka nje ya Tanzania
kupitia njia mbalimbali zikiwamo bandari
bubu za Bagamoyo, Tanga pamoja na mipakani kwa kutumia usafiri wa malori
makubwa ya mizigo ambayo hufanya safari zake katika nchi za Congo DRC, Kenya,
Zambia, Malawi na nchi nyingine.
Matokeo
ya utafiti huo unakuja huku kukiwa na katazo la Mamlaka ya Chakula na Dawa hapa
nchini (TFDA) kuhusu utumiaji, uingizwaji na uuzwaji wa vipodozi hivyo ambavyo
ni hatari kwa afya ya binadamu.
Ofisa
Uhusiano wa TFDA, Gaudensia Simwanza anasema kuwa mamlaka hiyo imepiga marufuku
vipodozi vyote vyenye viambata sumu, ingawa bado watu wanavitumia.
Katika
kutokomeza matumizi ya vipodozi vyenye viambata sumu Simwanza anasema TFDA
imeanza mpango wa kutoa elimu kwa wanafunzi ambao ni rahisi kuelimisha jamii
kutokana na elimu watakayoipata.
“TFDA
imebainisha baadhi ya vipodozi vyenye viambata sumu kuwa ni pamoja na Carolight,
inayotajwa kuwa na sumu kali zaidi pamoja na vile vyenye madini ya zebaki au mercury sabuni ya jaribu
na mekako clobetasol na betamethasone, krimu ya amira, betasol na skin success,”anasema.
Anasema
tafiti za kitaalamu zimeonyesha athari kubwa ya matumizi ya kemikali hizo hasa
kwa wanawake wajawazito kutokana na kemikali hizo kuathiri watoto wakiwa tumboni
na kuwasababishia watoto hao ulemavu,
saratani hata kifo mara wanapozaliwa.
Mkurugenzi wa idara ya kinga ya ORCI
Dk. Julius Mwaiselage anaitaja kemikali nyingine ya Butylated
hydroxyanisole (BHA) inayowekwa kwenye lipstiki
kuwa husababisha saratani ya ini na figo. Pia Polyethylene glycols ambazo
huwekwa kwenye krimu husababisha ugonjwa huo anasema.
Dk. Mwaiselage anasema changamoto
kubwa ambayo wanakutana nayo ni hali ya wanawake wengi ambao hutumia vipodozi
vilivyochanganywa kienyeji jambo ambalo ni vigumu kubaini aina halisi za
kemikali zilizotumika ndani yake.
“Wanawake
wanapaswa kuzingatia ushauri na elimu inayotolewa kuhusu hatari ya matumizi ya
kemikali, kuachana na tabia ya kutumia vipodozi duni na kufuata maelekezo
yaliyotolewa na TFDA ili kuepukana na matatizo ambayo siyo ya lazima,”anasema.
Dk.
Tara Cullis kwa Canada ambaye ni muasisi wa taasisi ya David Suzuki Foundation ya chuo
kikuu cha Harvard anasema kemikali ya BHA na Butylated hydroxytoluene BHT ni
kemikali ambazo huwekwa kwenye lipsticks pia husababisha mtumiaji kupata
saratani.
Mwalimu
wa Shule ya Wasichana ya Kisutu jijini Dar es Salaam Daniel Kibona anasema
ugonjwa wa saratani ya ngozi hauwezi kukoma hapa nchini kwasababu serikali
haijaweka misingi imara ya kukomesha matumizi ya vipodozi vyenye viambata sumu.
Kibona
anaongeza kuwa tatizo la matumizi ya vipodozi hivyo ni kubwa kwasababu
halijaingizwa katika mitaala ya kufundishia wanafunzi na hakuna kipengele cha
kufundisha juu ya madhara ya vipodozi kama ilivyo kwa magonjwa mengine ya malaria,
kipindupindu, kichocho na mengine ya zinaa.
Naye
mkazi wa Ilala Bungoni jijini humo, Zulfa Husein anasema chanzo cha utumiaji wa
vipodozi hivyo ni tamaa inayosababishwa na wanawake wenyewe kuhamasishana
kutumia mikorogo ili kutambiana urembo na kujikuta wakiharibu ngozi zao.
Rose Mkalimoto mkazi wa Kimara pia jijini Dar es Salaam
anasema baadhi ya wanawake wanatambua madhara yatokanayo na matumizi ya vipodozi hivyo licha ya kupatiwa elimu mara
kwa mara.
“Mimi
niliwahi kumshauri mwanamke mmoja aache kutumia mkorogo, matokeo yake alikuwa
mkali na kunikebehi kwa kuniita mshamba na ninamuonea wivu…hata ninapojaribu
kuwaasa wasichana na marafiki zangu
wengine hawanielewi kwasababu wameshajijengea kwamba uzuri wa mwanamke sharti
awe mweupe ,” anasema Mkalimoto.
Anasema katika kipindi hiki pia kuna baadhi ya
wanafunzi wa shule za sekondari ambao wamejiingiza kwenye matumizi ya vipodozi
hivyo kutokana na kukosa elimu juu ya madhara ya vipodozi vyenye viambata sumu
Bahati
Shukuru, ni miongoni mwa watumiaji wa vipodozi hivyo, anasema ni miaka mitano sasa anatumia vipodozi
hivyo lakini ngozi yake inapendeza na kusababisha rafiki zake kuitamani kwa
kiasi kikubwa.
“Mimi
natumia na hata marafiki zangu wamevutiwa na weupe wangu, hayo madhara yanaletwa na watu wanaotaka
kuvuruga biashara za wenzao mbona kuna
watu wanaugua saratani ya ini, utumbo, na hata ya shingo ya uzazi nao wamepaka
Carolite? anahoji Bahati.
Anasema
wanaoumia ni wale wanaotumia mkorogo wa jadi: “Wanachanganya dawa ya meno na
sabuni ya unga, jaribu pamoja na dawa ya kuondolea madoa kwenye nguo ‘jiki’,”anasema.
Dk.Elidje Ekra ambaye ni Mhadhiri wa
Chuo Kikuu cha Treichville Abidjan, nchini Ivory Coast, anasema idadi kubwa ya wanawake
wenye saratani ya ngozi nchini humo ilimfanya aamue kufanya utafiti uliogundua kwamba
waathirika walikuwa wakitumia mikorogo ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa kupata
ugonjwa huo.
Anasema kuwa kemikali zinazotumika
ili kuhakikisha ufanisi wa kuchubua rangi asili ya binadamu zinachangia kwa
kiasi kikubwa kuongezeka kwa matatizo ya shinikizo la damu pamoja na kisukari.
“Mikorogo inayochubua ngozi ni
maarufu mno katika mataifa mengi ya Afrika huku wanawake wengi wakipendelea
kujichubua ili waweze kukubaliwa kwamba ni warembo wanaovutia zaidi kumbe wanajitengenezea
sumu inayowatesa na kuwamaliza kabisa,”anasema.
Anabainisha
kuwa matumizi ya vipodozi hivyo yanachochewa na kasumba ya madai kwamba
mwanamke mrembo sharti awe na ngozi laini na nyeupe, pamoja na kuwaridhisha
wenzi wao wanaopenda wanawake weupe hali ambayo inazidi kuathiri wanawake kwa
kiasi kikubwa bila wao wenyewe kujua.
Taarifa
kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) inabainisha kuwa kati ya asilimia 100 ya
dawa duniani kote 10 kati yake ni bandia au duni na kwamba asilimia 50 ya dawa hizo
duni hutengenezwa kutoka nchini China na India ambako kuna maabara zilizoko chini
ya ardhi.
Dawa
hizo duni ni zile ambazo viambata vyake havikidhi viwango vya ubora
vinavyokubalika kisayansi pamoja na mtengenezaji wake kubadili viambata, nembo,
vifaa vya kufungashia na wengine hudanganya kwa namna yoyote ile kwa lengo la
kujipatia kipato.
TFDA inakiri tatizo kubwa la matumizi ya vipodozi vyenye kemikali hapa nchini licha ya kutoa elimu kwa njia mbalimbali ikiwamo kwenye mihadhara na maonesho kama vile ya wakulima Nane nane, Sabasaba na mengine.
TFDA inakiri tatizo kubwa la matumizi ya vipodozi vyenye kemikali hapa nchini licha ya kutoa elimu kwa njia mbalimbali ikiwamo kwenye mihadhara na maonesho kama vile ya wakulima Nane nane, Sabasaba na mengine.
Matumizi
ya vipodozi vyenye viambata sumu yanazidi kuteketeza nguvu ya Taifa kutokana na
ongezeko la ugonjwa wa saratani, hivyo ni jukuu la kila Mtanzania kumwelimisha mwenzake
ili kuepukana na ongezeko hilo.
Pia serikali inapaswa
kuhakikisha inaongeza kipengele cha vipodozi na madhara yake katika mitaala ya
mafunzo kwa shule za msingi na sekondari ili kuhakikisha janga hilo linapungua
na kutokomea kabisa. CHANZO: TAIFA LETU
COMMENTS