Na Mwandishi Wetu, Kilwa MBUNGE wa jimbo la Kilwa Kusini anayemaliza muda wake, Seleman Bungara, amesema safari hii atamshinda kwa ...
Na Mwandishi Wetu, Kilwa
MBUNGE wa jimbo la Kilwa Kusini anayemaliza muda wake,
Seleman Bungara, amesema safari hii atamshinda kwa kura za kishindo mgombea
mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hasnain Dewji aliyeshinda kura za maoni
ndani ya chama hicho tawala.
Mgombea huyo maarufu kama Bwege aliyesimama kwa mwamvuli wa
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), amesema ushindi huo utachagizwa zaidi ya
Ukawa ambapo mwaka 2010 alipata kura 14,610 dhidi ya aliyekuwa mgombea wa CCM
wakati huo, Ramadhan Madabida aliyepata kura 14,028.
Madabida ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es
Salaam alipata nafasi ya kugombea 2010 baada ya kumshinda Dewji katika kura za
maoni baada ya kuongoza jimbo hili mwa msimu mmoja wa mwaka 2005 hadi 2010.
Akizungumza na SEMA Usikike jana, Bwege amesema
amefarijika mno kuona CCM imemteua Dewji kupambana naye Oktoba 25 na kwamba
atamshinda kirahisi tena kwa kura nyingi kwa sababu uchaguzi wa mwaka huu
utatawaliwa zaidi na nguvu ya Ukawa.
"CCM kumteua Dewji ni kama vile inatapatapa,
haiwezekani aonekane hafai mwaka 2010 na wakamtosa katika kura za maoni halafu
leo aje kuwa lulu kwao, wananchi wa Kilwa wataonyesha ukomavu wao kisiasa
katika hiki kwa kumkataa Dewji aliyetumwa na CCM," alisema.
Alisema anajua fika
kuwa, Dewji atajaribu kufurukuta ili kusaka ushindi, lakini nguvu ya Ukawa
itamshughulikia ipasavyo na kusisitiza kuwa labda CCM ingemrudisha tena
Madabida angesumbua kidogo.
Dewji mwenyewe hakupatikana kuzungumzia alivyojipanga baada
ya kampeni kuanza rasmi jana kote nchini, ingawa habari kutoka ofisi za CCM
wilaya ya Kilwa zinasema, mkakati uliowekwa mwaka huu hautampa nafasi Bwege
kutetea kiti chake.
Mbali na Bwege na Madabida vyama vingine vilivyogombea
ubunge jimbo la Kilwa Kusini mwaka 2010 ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) kilichopata kura 287, NRA (91), NLD kura 79.
COMMENTS